0
Wazambia wajitokeza kwa wingi kumpigia rais kuraWananchi wa Zambia wamejitokeza kwa wingi kupiga kura katika uchaguzi wa rais atakayechukua nafasi ya hayati Michael Sata ambaye alifariki dunia mjini London mwezi Oktoba mwaka uliopita. Kumeripotiwa mvua kali katika aghalabu ya maeneo ya Zambia lakini watu walijitokeza baadaye mchana katika masanduku ya upigaji kura. Hali imeripotiwa kuwa ni shwari huku uchaguzi ukifanyika kwa amani. Mgombea wa chama tawala cha Patriotic Front (PF) Edgar Lungu mwenye umri wa miaka 58 na ambaye pia ni Waziri wa Ulinzi kwa sasa ana matumaini ya kupata ushindi katika uchaguzi wa leo. Licha ya kuweko wagombea kadhaa wanaowania kiti hicho, lakini Hakainde Hichilema mgombea wa chama cha upinzani cha UPND anatajwa kuwa mpinzani mkuu wa Edgar Lungu katika uchaguzi wa leo. Tume ya uchaguzi ya Zambia imetangaza kuwa, zoezi la kuhesabu kura litaanza muda mfupi tu baada ya zoezi la upigaji kura kukamilika. Taarifa ya tume hiyo imeeleza kuwa matokeo ya uchaguzi huo yanatarajiwa kutangazwa katika kipindi cha masaa 48. Mwangalizi mkuu wa uchaguzi kutoka Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika SADC Maite Nkoana Mashabane amepongeza kujitokeza idadi kubwa ya wapiga kura ambao walikuwa na subira. . Hivi sasa nchi hiyo inaongozwa na aliyekuwa makamu wa rais wa Sata,  Guy Scott Mzambia mzungu, ambaye kutokana na kwamba wazazi wake walizaliwa nje ya nchi hiyo, amezuiliwa kugombea katika uchaguzi huo.

Post a Comment

 
Top