0
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira amesema ubora wa mgombea ndiyo utakaokuwa msingi wa ushindi katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Desemba 14 na Uchaguzi Mkuu 2015.
Akizungumza mjini Arusha mwishoni mwa wiki, Wasira anayetajwa kuwa mmoja wa watu wanaowania kuteuliwa kugombea urais kupitia CCM, alisema hakuna chama kitakachoshinda kwa kutegemea umaarufu wake au wingi wa wanachama wake.
Alisema upigaji kura ungekuwa unazingatia chama, basi CCM isingehangaika kupiga kampeni na kujinadi kwani ndicho chenye wanachama wengi nchini na hivyo kingeshinda kirahisi.
Utafiti wa Twaweza
Akijibu swali la nini maoni yake kuhusu utafiti wa Taasisi ya Twaweza kuhusu urais mwakani, Wasira alisema: “Kwanza sijausoma utafiti wenyewe kujua vigezo na sampuli ya utafiti wao, lakini lililodhahiri ni kwamba ubora wa mgombea au wagombea ndiyo msingi wa ushindi kwenye uchaguzi.”
Waziri huyo aliyekuwa jijini Arusha kuhudhuria vikao vya CCM kupitia nafasi yake ya ulezi wa chama hicho Mkoa wa Arusha alisema kipindi cha viongozi kufikiria ukubwa na umaarufu wa vyama vyao nyakati za kampeni na uchaguzi kimepitwa na wakati, badala yake kila chama lazima kiwapime, kuwachuja na kupata wagombea bora.
“Ndani ya CCM tayari tumebaini hilo ndiyo maana tuko makini kwenye uteuzi wa wagombea wa nafasi mbalimbali kuanzia chaguzi za ndani na nje ya chama,” alisema.
Alisema CCM na viongozi wake wanaujua ukweli huo kuwa wananchi hawaangalii itikadi zao za vyama wakati wa kupiga kura, bali ubora wa mgombea. “Wananchi hawapigi kura kwa kuzingatia uanachama wa vyama vyao. Hapana! Wanaangalia ubora wa mgombea. Mgombea bora hushinda hata kama chama chake kina wanachama wachache katika eneo husika,” alisema na kuongeza:
“Nawatoa hofu wanaCCM kuhusu uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Ukuu mwakani. Chama kitasimamisha wagombea bora ili kujihakikishia ushindi kama uchaguzi uliopita.”
Azungumzia Ukawa
Akijibu swali la iwapo CCM imeingiwa hofu ya kushindwa kwenye chaguzi kuanzia Serikali za Mitaa baada ya vyama vikuu vya upinzani nchini vya kuungana na kuunda Ukawa, Wasira alijibu kwa kejeli akisema:
“Hakuna anayekatazwa kuota ndoto. Kuota ndoto ni jambo la kawaida na kila mtu anaruhusiwa kuota. Ila ukweli unabaki kuwa ndoto ni ndoto tu, ndiyo maana anayeota akiamka hutambua kuwa alikuwa ndotoni.”

Post a Comment

 
Top